0%

https://uongofu.com/wp-content/uploads/2021/06/services-head-1.png

ADABU ZA KUINGIA CHOONI

ADABU ZA KUINGIA CHOONI

Suali: Ni zipi adabu za kuingia chooni?

Jawabu: Hakika dini ya kiislamu haikuwacha kitu katika mambo ya kheri ila imewafundisha waislamu,na hakuna jambo lolote la shari ila limewatahadharisha waislamu. Kiasi hata mtu anapotaka kwenda chooni pia limefundisha adabu zake na huu ndio uzuri wa dini hii ya kiislamu hata makafiri walishangazwa na dini hii. Mpaka mmoja katika washirikina alimuuliza Salmaan Al-Faarisy ya kuwa Mtume wenu amewafunza kila kitu hata pia kwenda chooni? Salmaan akamwambia ndio ametukataza kuelekea kibla wakati wa kukidhi haja kubwa au ndogo. Hadithi hii imepokewa na Al-Tirmidhy,na akasema na hadithi Swahihi na asli yake iko katika swahihi Muslim.
Na katika adabu zilowekwa na sheria mtu anapo taka kwenda haja ni hizi zifuatavyo:
1 . Asielekee kibla wakati anapo taka kuingia choni sawa iwe ni haja ndogo ama haja kubwa na huku ni katika kuhishimu Al-Kaaba na ni katika kuhishimu ibaada ya Mwenyezi Mungu (S.W.) na dalili ya hili, ni neno lake Mtume ﷺ:

[إِذَا جَلَسَ أَحَدُكُمْ عَلَى حَاجَتِهِ فَلا يَسْتَقْبِلْ الْقِبْلَةَ وَلا يَسْتَدْبِرْهَا]      رواه مسلم 

[Atakapo kaa mmoja wenu kutaka kukidhi haja yake basi asieleke kibla wala asikipe Maungo]   [Imepokewa na Muslim]

2. Asiguse tupu yake kwa mkono wa kulia na huku yuwakojoa kwa neno lake Mtume Muhammad ﷺ:

[ إِذَا بَالَ أَحَدُكُمْ فَلا يَأْخُذَنَّ ذَكَرَهُ بِيَمِينِهِ وَلا يَسْتَنْجِي بِيَمِينِهِ وَلا يَتَنَفَّسْ فِي الإِنَاءِ .]    رواه البخاري

[Anapo kojoa Mmoja wenu asishike Dhakari yake kwa mkono wake wakulia wala asitambe kwa Mkono wake wakulia. Wala asivuvie kwenye chombo (wakati anapo kunwa) ]    [Imepokewa na Bukhari]

3. Asiondoshe najisi kwa Mkono wake wakulia bali atumie mkono wake wakushoto,kwa hadithi ilio tangulia na kwa neno lake Mtume ﷺ :

[ إِذَا تَمَسَّحَ أَحَدُكُمْ فَلا يَتَمَسَّحْ بِيَمِينِهِ .]     رواه البخاري

[Anapo Jipangusa Mmoja wenu basi asijipanguse kwa mkono wake wakulia]  Imepokewa na Bukhari, na kwa hadithi ilio pokelewa na bibi Hafswa mke wa Mtume (S.A.W.)

أنَّ النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ كَانَ يَجْعَلُ يَمِينَهُ لأَكْلِهِ وَشُرْبِهِ وَوُضُوئِهِ وَثِيَابِهِ وَأَخْذِهِ وَعَطَائِهِ وَيَجْعَلُ شِمَالَهُ لِمَا سِوَى ذَلِكَ . رواه الإمام أحمد وهو في صحيح الجامع 4912

[Kwamba Mtume ﷺ Alikuwa akijalia mkono wake wakulia kwa ajili ya kula na kunywa na kutawadhia na kuvalia nguo na kuchukuwa na kupeana. Akijalia mkono wake wakushoto kwa yasio kuwa hayo]     [Imepokewa na Imam Ahmad katika Swahihul- jaami’a]

4. Na ni sunna Akidhi haja yake akiwa amekaa na hali yakuwa amejikurubisha na ardhi kwa kufanya hivyo huwa atajiaminisha na tetezi za mikojo na pia ni katika kujisitiri asipate kuonekaniwa lakini akiwa yuko sehemu ambao atapokuwa amekaa atajipaka najisi basi anaruhusiwa kukojowa kwa kusimama.

5. Ajistiri na kuonekaniwa na watu wakati anapotaka kwenda haja; na mtu atapokuwa kwenye Jangwa na akataka kwenda chooni na asipate kitu cha kujisitiri,basi ni aende mbali na watu kwa hadithi ilio pokelewa na Mughira bin Shu’ba asema nilikuwa na Mtume ﷺ Safarini ,mtume akataka kwenda kukidhi haja basi alikwenda mbali. Hadithi hii imepokwa na imam Al-Ttirmidhi

6. Asiinuwe nguo yake ila baada ya kusongea kwenye Ardhi na huku ni katika kujisitiri,kwa hadithi iliopokelewa na Anas (R.A) Asema [alikuwa Mtume rehma na amani zimfikie yeye anapo taka kwenda haja hainui nguo yake mpaka akurubie katika Ardhi] imepokewa na Al-Ttirmidhiy.
Na akiingia chooni asiinuwe nguo yake ila baada ya kufunga Mlango na huku ndiko kujisitiri sio kama wanavyofanya wasio kuwa waislamu kukidhi haja zao mbele ya watu bila ya kuona haya.

7. Na katika adabu ya kuingia choni ni kusoma dua ziliofunzwa na bwana Mtume rehma na amani zifikie yeye mtu anapotaka kwenda chooni wakati wa kuingia na wakati wakutoka.
Ametufunza mtume ﷺ Aseme Mmoja wetu anapo taka kwenda chooni, aseme

[بسم الله ، اللهم إني أعوذ بك من الخبث والخبائث]

[Kwa jina la Mwenyezi Mungu,Ewe Mola wangu najilinda kwako na Mahsetani wa kiume na wakike]

Na wakati wakutoka amuomba Mwenyezi Mungu Msamaha kwa kusema:

[غفرانك]

“Msamaha ni wako wewe”

8. Kuchunga na najisi kwa kujisafisha vizuri baada ya kumaliza haja yake. Kwa tahadhari iliotolewa na Mtume ﷺ Kwa wale wanao fanya usahali wakijitwahirisha na mikojo; Asema Mtume ﷺ:

[ أَكْثَرُ عَذَابِ الْقَبْرِ مِنْ الْبَوْلِ]     رواه ابن ماجة

[Wingi wa Adhabu ya kaburi yatokamana na Mikojo]
Kwa wale wasiojisafisha vizuri na kufanya usahali wa hilo.

9. Ajisafishe na najisi au kujipangusa Mara tatu na akihitajia zaidi basi afanye witri,mara tano au saba au tisa namna hivyo. Kama ilivyo kuja katika hadihti ya bibi Aisha Radhi za Mungu ziwe juu yake asema alikuwa Mtume Rehma na amani akijisafisha mara tatu] hadithi hii imepokewa na Ibnu Maajah.
Na kwa hadithi ilio pokewa na Abuu Hureyra (R.A.) asema:

]إِذَا اسْتَجْمَرَ أَحَدُكُمْ فَلْيَسْتَجْمِرْ وِتْرًا ]    رواه الإمام أحمد وحسنه في صحيح الجامع

Amesema Mtume Rehma na Amani zimfike yeye, [Anapotumia mawe Mmoja wenu (kwa ajili ya kujisafisha) basi ajisafishe Witri]     [Imepokewa na Imam Ahmad]

10. Anapo tamba kwa Mawe basi asitumie Mfupa wala choo cha Mnyama Wala koko za vitu vinavyliwa kama koko ya maembe na kadhalika kwa sababu ni chakula ni lazima kihishimiwe.

11. Asikojoe kwenye maji yalio tulia kwa hadithi iliopokewa na Jabir (R.A) Asema:

[لما رواه جَابِر رضي الله عنه عَنْ رَسُولِ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ أَنَّهُ نَهَى أَنْ يُبَالَ فِي الْمَاءِ الرَّاكِدِ .] ” رواه مسلم

[Amekataza Mtume ﷺ kukojolewa kwenye maji yalio tulia]     [Imepokewa na Muslim.]

Kwa sababu kufanya hivyo ni kuyanajisha Maji,na kuwaudhi watumiaji wa maji hayo.

12. Asikidhi haja yake kwenye njia au kwenye kivuli watu wanajimpumzisha. Kwa sababu kufanya hivyo ni kuudhi watu na amepokea Abuu Hurayra (R.A.) Kutoka kwa Mtume Rehma na amani zimfikie yeye amesema:

[اتَّقُوا اللاعِنَيْنِ قَالُوا وَمَا اللاعِنَانِ يَا رَسُولَ اللَّهِ قَالَ الَّذِي يَتَخَلَّى فِي طَرِيقِ النَّاسِ أَوْ ظِلِّهِمْ]     رواه أبو داود

[Ogopeni vitu viwili vyenye kusababisha kulaniwa ? wakasema ni vitu gani hivyo ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu? Akasema ni kuingia chooni kwenye njia ya watu au kwenye kivuli chao]     [Imepokewa na Abuu Daud.]

13. Asimsalimie mtu anae kidhi haja yake, wala Asirudi salaamu wakati anapo kidhi haja, na huku ni kuhishimu jina la Mwenyezi Mungu Subhanahu wata’aala kutotajwa kwenye sehemu zinazo chukiza.

عَنْ جَابِرِ بْنِ عَبْدِ اللَّهِ أَنَّ رَجُلًا مَرَّ عَلَى النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ وَهُوَ يَبُولُ فَسَلَّمَ عَلَيْهِ فَقَالَ لَهُ رَسُولُ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ إِذَا رَأَيْتَنِي عَلَى مِثْلِ هَذِهِ الْحَالَةِ فَلَا تُسَلِّمْ عَلَيَّ فَإِنَّكَ إِنْ فَعَلْتَ ذَلِكَ لَمْ أَرُدَّ عَلَيْكَ .    رواه ابن ماجة

Amepokea Jabir bin Abdillah (R.A) Kwamba Mtu moja alipita kwa mtume akiwa anakojowa akamsalimia. Mtume ﷺ alimwambia [Ukiniona mimi katika hali hii usinisalimie kwa sababu ukifanya hivyo (ukanisalimia)  sitaitikia salamu yako]     [Imepokewa na Ibn Maajah.]
Na jamhuri ya wanachuoni wasema ni Makruhi mtu kuzungumza wakati anapo kidhi haja yake.

Hizi ndizo adabu zilowekwa na sheria na kuhimiza kila Muislamu awe ni mwenye kuzifuata kwa sabubu ni jambo lamtokea kila mtu na kila siku.

Na Allah ndie mjuzi zaidi.


Toa maoni yako

Begin typing your search above and press return to search.