0%

https://uongofu.com/wp-content/uploads/2021/06/services-head-1.png

UMUHIMU WA TAWHIDI NA FADHALA ZAKE

UMUHIMU WA TAWHIDI NA FADHALA ZAKE

Tawhidi ni sababu ya kuokoka mwanadamu siku ya kiama na pia kubainisha kwamba Tawhidi ni sababu ya kuondoshewa balaa na fitna
Tawhidi ni msingi mkubwa ambao Mwenyezi Mungu amewaumba majini na watu kwa ajili yake. Kwani Mwenyezi Mungu hakuwaumba majini na watu isipokuwa kwa kumuabudu yeye. Amesema Mwenyezi mungu (Subhaanahu wa Taala):

{وَمَا خَلَقْتُ الْجِنَّ وَالْإِنسَ إِلَّا لِيَعْبُدُونِ}   الذريات:56

[Sikuwaumba majini na watu isipokuwa waniabudu ]   [Addhariyati : 56].

Tawhidi ni jambo kubwa. Allah Subhaanahu wa Taala Amelibainisha katika kitabu chake na pia Mtume, rehma na amani zimfikie ameliweka wazi katika hadithi zake tukufu.Tawhidi ni jambo ambalo hawezi kuokoka mtu yoyote duniani na kesho Akhera ila alikamilishe jambo hilo la kumpwekesha Mwenyezi Mungu na kutomshirikisha na chochote. Amesema Mtume :

[من مات وهو يعلم أن لا إله إلا الله دخل الجنة]     رواه مسلم

[Atakaye kufa na akijua ya kwamba hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa Mwenyezi Mungu ataingia peponi].    [Imepokewa na Muslim]

UMUHIMU WA TAWHIDI

Tawhidi ni jambo bora sana, na kwa sababu hii Allah (Subhaanahu wa Taala) Ameshuhudia kwa nafsi yake vile vile Malaika wameshuhudia na pia waliopewa ilimu. Na hii ni kuonesha ubora wa jambo hili la Tawhidi. Jambo Amelishuhudilia Mwenyezi Mungu(Subhaanahu wa Taala), wakashuhudia Malaika watukufu na pia wanadamu watukufu na watu waliopewa ilimu.Amesam Mwenyezi Mungu Subhaanahu wa Ta’aala

{شَهِدَ اللَّهُ أَنَّهُ لَا إِلَٰهَ إِلَّا هُوَ وَالْمَلَائِكَةُ وَأُولُو الْعِلْمِ قَائِمًا بِالْقِسْطِ ۚ لَا إِلَٰهَ إِلَّا هُوَ الْعَزِيزُ الْحَكِيمُ}    آل عمران:18

[Ameshuhudia Mwenyezi Mungu ya kwamba hapana mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa yeye na Malaika na pia waliopewa ilimu,hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa yeye Mwenye nguvu Mwenye hekima.]   [Al-Imran : 18 ].

Miongoni mwa umuhimu wa Tawhidi ni kwamba Mtume ﷺ Alilingania Tawhidi kuanzia mwanzo wa ulinganizi wake hadi mwisho wa uhai wake, bali Mitume wote walilingania hivyo.
Pia tunapata katika sira ya Mtume ﷺ ya kwamba alipokuwa akituma maswahaba kwenda kulingania katika sehemu fulani huwausia kwanza kuwalingania watu katika Tawhidi. Yaani (Kumpwekesha Mwenzi mungu s.a)
Miongoni mwa umuhimu wa Tawhidi ni kwamba mwenye kushikamana na Tawhidi husamehewa dhambi zake na anaepushwa kukaa motoni.
Mwenye kushikamana na Tawhidi huwa karibu zaidi na Mwenyezi Mungu na pia hupata amani kamili na uongofu hapa duniani na kesho akhera.Mwenyezi Mungu Amesema (Subhaanau wa Ta’aala)

{الَّذِينَ آمَنُوا وَلَمْ يَلْبِسُوا إِيمَانَهُم بِظُلْمٍ أُولَٰئِكَ لَهُمُ الْأَمْنُ وَهُم مُّهْتَدُونَ}     الأنعام:82

[Wale ambao wameamini, na hawakuchanganya imani yao na dhulma – hao ndio watakao pata amani na wao ndio walio ongoka.]    [Al-Anaam : 82].

Kwa mujibu wa Aya hii ni kwamba Muislamu anayeshikamana na Tawhidi atakuwa na amani hababaiki hapa duniani yuwajua litakalompata hapa duniani ni kadari ya Mola (Subhaanahu wa Taala) na kuwa atapata amani kesho akhera.
Bila ya kusahau kuwa endapo waumini watashikamana na tauhudi wataondoshewa balaa na fitna kesho akhera. Amesema Mtume ﷺ:

من شهد أن لا إله إلا الله وأن محمداً عبده ورسوله، وأن عيسى عبد الله ورسوله، وكلمته ألقاها إلى مريم وروح منه، والجنة حق، والنار حق؛ أدخله الله الجنة على ما كان من العمل     رواه البخاري ومسلم

[Anayeshuhudia ya kwamba hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki isipokuwa yeye asiyekuwa na mshirika na Muhammad ni Mtume wa Mwenyezi Mungu na kwamba Nabii Isa ni mja wa Mwenyezi Mungu na Mtume wake na neno lake alilolitia kwa Mariam na roho kutoka kwake na pepo ni haki na moto ni haki Mwenyezi Mungu atamwingiza peponi kulingana na amali].   [Imepokewa na Bukhari na Muslim]

Ni vyema niwatajie mifano ya ambao waliepushiwa balaa na fitna.Tutoe mfano katika Mitume walioepushiwa balaa na fitna ni Nabii Ibrahiim pale walipokuwa watu wake wanataka kumchoma Mwenyezi Mungu Alimwokoa kwa kuuambia moto: “Ewe moto kuwa baridi na salama kwa Ibrahim” na ikawa kama alivyotaka Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala). Na Mtume mwengine ni Nabii Lut pale Mwenyezi Mungu Alipowaangamiza watu wake na kumwokoa yeye na waliomwamini yeye, na mifano ya walioepushiwa balaa na fitna ni mingi sana.

AINA YA TAWHIDI

Tawhidi inagawanyika sehemu tatu :
1. Tawhidu-Arrububiyah.
Tawhidi ya vitendo vya Mwenyezi Mungu s.a. nayo ni kumpwekesha Mwenyezi mungu katika uumbaji na uendeshaji wa mambo ya viumbe, na hashirikiani na yoyote katika hilo yoyote.Mwenyezi mungu anasema:

اللَّهُ الَّذِي خَلَقَ السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضَ وَأَنزَلَ مِنَ السَّمَاءِ مَاءً فَأَخْرَجَ بِهِ مِنَ الثَّمَرَاتِ رِزْقًا لَّكُمْ ۖ وَسَخَّرَ لَكُمُ الْفُلْكَ لِتَجْرِيَ فِي الْبَحْرِ بِأَمْرِهِ ۖ وَسَخَّرَ لَكُمُ الْأَنْهَارَ    إبراهيم:32

[Mwenyezi Mungu ndiye aliyeumba mbingu na ardhi na ameteresha kutoka mawinguni maji akatoa kwa maji hayo mazao hali yakuwa ni riziki kweni nyinyi na akawadhalilishia majahazi ili yapite katika bahari kwa amri yake, na akawadhalilishia nyinyi mito ya maji ] [Ibrahim: 32 ].

2. Tawhidul-Uluuhiya. Nayo ni:
Tawhidi ya kumpwekesha Mwenyezi Mungu katika ibada. Maana ya maneno haya ni kwamba Mwenyezi Mungu Ndiye Anayefa kuabudiwa peke yake,wala haifai kushirikishwa na yoyote.Mwenyezi Mungu (Subhaanhu wa Ta’aala)

{إِيَّاكَ نَعْبُدُ وَإِيَّاكَ نَسْتَعِينُ}    الفاتحة:5

[Ni wewe tu tunakuabudu na kwako wewe peke yako tunataka msaada]   [Al-Faatiha : 5].

3. Tawhidul-Asmaai wa Swifaat.
Tawhidi ya kumpwekesha Mwenyezi Mungu katika Sifa Zake na majina yake. Maana yake ni kwamba Mwenyezi Mungu hafanani na yoyote katika Sifa Zake na majina yake .Wala hafai yoyote kujifananisha wala kumfananisha yoyote na Mwenyezi Mungu katika sifa au majina yake kwani hana mfano wa yoyote.Asema Mwenyezi Mungu Subhaanahu wa Ta’aala

{قُلْ هُوَ اللَّهُ أَحَدٌ اللَّهُ الصَّمَدُ لَمْ يَلِدْ وَلَمْ يُولَدْ وَلَمْ يَكُن لَّهُ كُفُوًا أَحَدٌ}    الإخلاص:1-4

[Sema; Mwenyezi Mungu ni mmoja Mwenyezi Mungu Ndiye Anayetakwa msaada, hakuzaa wala hakuzaliwa na Hana mfano Wake yoyote”]   [Al-Ikhlas 1 – 4].

Aina zote za Tawhidi ni lazima kwa Muislamu azijue na azitumie katika maisha yake na hii ni kwa faida ya Muislamu. Na endapo mtu ataenda kinyume na aina hizi za Tawhidi basi ameshajitia matatizo duniani na kesho akhera, kwani Mwenyezi Mungu hamsamehe anayekufa katika shirki bila yakutubai.

{إِنَّ اللَّهَ لَا يَغْفِرُ أَن يُشْرَكَ بِهِ وَيَغْفِرُ مَا دُونَ ذَٰلِكَ لِمَن يَشَاءُ ۚ وَمَن يُشْرِكْ بِاللَّهِ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا بَعِيدًا}   النساء:116

[Hakika Mwenyezi Mungu hasamehi kushirikishwa na kitu. Lakini Yeye husamehe yasiyo kuwa hayo kwa amtakaye. Na anaye mshirikisha Mwenyezi Mungu basi huyo amepotea upotovu wa mbali].  [An-Nisaa : 116].

MAMBO YANAYO HARIBU TAWHIDI

Miongoni mwa mambo ambayo yanatakiwa ajitahadhari nayo muislamu yasije yakamtia katika matatizo hapa dunaini na kesho akhera.
1. Ushirikina kwa aina zake zote. Kwani shirki kubwa inafutilia mbali imani ya tawhidi.
Na shirki ndogo ina punguza ukamilifu wa Tawhidi.Na mfano wa shirki ni kumuomba asiyekuwa Mwenyezi Mungu jambo ambalo hana uwezo nalo isipokuwa Mwenyezi Mungu.
A. Na katika shirki kubwa ambayo tunayaona leo ni kufanya tawaf katika makaburi, (kuyazunguka makaburi)
B. kwenda kwa waganga na wachawi bali kuyaamini yote wanayoyasema kwa kudai mambo yaliofichika, na uhakika ni kwamba hakuna anayejuwa yaliofichika isipokuwa Mwenyezi Mungu na hakuna anayeweza kuleta madhara kumpata mtu isipokuwa Mwenyezi Mungu na hakuna anayeweza kuzuia kheri Akitaka Mwenyezi Mungu kuleta kheri hiyo,Mwenyezi mungu anasema:

{وَإِن يَمْسَسْكَ اللَّهُ بِضُرٍّ فَلَا كَاشِفَ لَهُ إِلَّا هُوَ ۖ وَإِن يَمْسَسْكَ بِخَيْرٍ فَهُوَ عَلَىٰ كُلِّ شَيْءٍ قَدِيرٌ}   الأنعام:17

[Na ikiwa Mwenyezi Mungu akikugusisha madhara, basi hapana wa kukuondolea hayo ila Yeye. Na ikiwa akikugusisha kheri, basi Yeye ndiye Mwenye uweza wa kila kitu.]   [ Al-Anaam : 17].
Kwa hivyo, tujue ya kwamba Mwenyezi Mungu Ndiye anayeleta manufaa na madhara, na kwa sababu hiyo yatakiwa Mwenyezi Mungu aogopewe haki ya kuogopewa.
C. Na aina za shirki ni mtu kuomba dua kumuomba mtu jambo ambalo hakuna awezaye kulifanya isipokuwa Mwenyezi Mungu kama kuondoa ugonjwa. Huku tukijua ya kwamba dua ni ibada, kwa hivyo, ibada hiyo ya dua haifai kufanyiwa asiyekuwa Mwenyezi Mungu.
D. Aina nyingine ya shirki kubwa ni ushirikina katika nia na makusudio, hii ni mtu kunuwia au kufanya ibada kwa kutaka au kukusudia mambo ya kidunia au wamuone kwamba yuwafanya ibada au watu wamsikie au apate sifa kwa watu,Mwenyezi Mungu anasema:

مَن كَانَ يُرِيدُ الْحَيَاةَ الدُّنْيَا وَزِينَتَهَا نُوَفِّ إِلَيْهِمْ أَعْمَالَهُمْ فِيهَا وَهُمْ فِيهَا لَا يُبْخَسُونَ أُولَٰئِكَ الَّذِينَ لَيْسَ لَهُمْ فِي الْآخِرَةِ إِلَّا النَّارُ ۖ وَحَبِطَ مَا صَنَعُوا فِيهَا وَبَاطِلٌ مَّا كَانُوا يَعْمَلُونَ     هود:15-16

[Wanao taka maisha ya dunia na pumbao lake tutawalipa humo vitendo vyao kaamili. Na wao humo hawatopunjwa. Hao ndio ambao hawatakuwa na kitu Akhera ila Moto, na yataharibika waliyo yafanya, na yatapotea bure waliyo kuwa wakiyatenda.]    [Huud : 15 – 16].
Haya ni malipo ya wanaofanya ibada kwa ajili ya kuonekana na watu na kwa ajili ya dunia.
E. Aina nyingine ni shirki ya kutii viongozi wa dini kinyume na miongozo sahihi ya Uislamu katika kuhalalisha vilivyoharamishwa na Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala).

{اتَّخَذُوا أَحْبَارَهُمْ وَرُهْبَانَهُمْ أَرْبَابًا مِّن دُونِ اللَّهِ}    التوبة:31}

[Wamewafanya makuhani wao na wamonaki wao kuwa ni marabi badala ya Mwenyezi Mungu,]     [Tawba : 31].
Mtume ﷺ Alimfasiria Adiy bin Hatiim ibada yenu kwao ni kumtii katika kumuasi Mwenyezi Mungu (Subhaanahu wa Taala).kuhalalisha yalio haramiswa na Mwenzi Mungu.

KWA FAIDA ZAIDI SIKILA MADA HII NA SHEIKH SHADDAD

Toa maoni yako

Begin typing your search above and press return to search.