0%

https://uongofu.com/wp-content/uploads/2021/06/services-head-1.png

ITIKADI YA MASHIA KUHUSU KUZURU NAJAF NA KARBALAA

NI IPI ITIKADI YA MASHIA KUHUSU NAJAF NA KARBALAA, NA JE, KUNA FADHLA GANI KATIKA KUZURU SEHEMU HIZO ?

Mashia wanaitakidi sehemu yalipo makaburi ya watu waliodai kuwa ni Maimamu wao, au ambao ni Maimamu kweli, kwa sehemu hizo ni sehemu takatifu, hivyo Al-Kuufa ni haram (sehemu takatifu), pia Karbalaa ni haram, na Qumm nayo ni haram. Na wanayo riwaya wanayodai kuwa imepokelewa kwa As-Swaadiq kwamba, Allaah Anayo haram Yake ambayo ni Makkah, na Mtume Wake anayo haram yake ambayo ni Madiynah, na Amiyrul-Muuminiyna (´Aliy) anayo haram yake ambayo ni Al-Kuufah, na sisi tunayo haram yetu ambayo ni Qumm.

Na Kar-balaa kwa Mashia ni bora kuliko Al-Ka´abah. Imekuja katika Kitabu ‘Bihaarul-Anwaar’ kutoka kwa Abu ´Abdillaah kwamba kasema:
“Hakika Allaah Aliiteremshia Al-Ka´abah wahyi (ufunuo) lau kama si udongo wa Karbalaa nisingelikufanya bora, na lau kama si mwili wa yule aliyeko katika udongo wa Karbalaa nisingekuumba, wala nisingeumba nyumba ambayo kwayo umejifakharisha, basi tulia na uwe ni Mkia dhalili na si mwenye kibri kwa ardhi ya Karbalaa, la sivyo nitakutupa katika Jahannam.”(1)
Bali Raafidhwah wanaona kuzuru kaburi la Husayn huko Karbala ni bora kuliko nguzo ya tano ya Uislamu (Hijjah)!!

Amesema Al-Majlisiy katika kitabu chake ‘Bihaarul-Anwaar’ kutoka kwa Bashiyr Ad-Dahaan amesema: “Nilimuuliza Abu ´Abdillaah: “Endapo itanipita Hijjah kisha nikaenda katika kaburi la Husayn? Akasema: Vizuri sana ewe Bashiyr, Muumini yeyote atakaeliendea kaburi la Husayn hali ya kutambua haki yake, katika siku ambayo si siku ya ‘Iyd, basi huandikiwa thawabu za Hijjah 20 na ´Umrah 20 zenye kukubaliwa, na thawabu za kushiriki katika vita 20 vya Jihaad pamoja na Mtume au Imamu muadilifu, na atakayeliendea siku ya ´Arafah hali ya kujua haki zake basi huandikiwa thawabu za Hijjah 1000 na ´Umrah 1000 zenye kukubaliwa, na thawabu za kupigana Jihaad 1000 pamoja na Mtume au Imamu muadilifu.

Pia katika kitabu hicho hicho wametaja kwamba wanaozuru kaburi la Husayn huko Karbalaa ni watu safi, na wanaokuwa wamesimama ´Arafah ni watoto wa Zinaa!!
Imepokewa toka kwa ´Aliy bin Asbaatw kwamba kapokea toka kwa Abu ´Abdillaah kuwa kasema: “Hakika Allaah Mtukufu Anaanza kuwatazama wanaozuru kaburi la Husayn usiku wa kuamkia ´Arafah. Akasema: Nikamuuliza, kabla hajawatazama walioko katika kisimamo cha ´Arafah? Akasema: Ndio, nikamuuliza, kwanini iwe hivyo? Akasema: “Kwa sababu katika watu walioko ´Arafah mna watoto wa zinaa tofauti na wale walioko Karbalaa hakuna mtoto wa zinaa kati yao.”(2)

Bali kiongozi wao mkuu (wa hivi sasa) ´Aliy As-Sistaaniy katika kitabu chake ‘Minhaajus-Swaalihiyn’ amefadhilisha kuswali katika makaburi kuliko kuswali katika Misikiti!!
Kasema katika mas-alah nambari 562: “Inapendeza kuswali katika makaburi ya Maimamu (´Alayhimus-Salaam) bali imesemekana kuwa ni bora kuliko kuswali Misikitini, na imepokewa kwamba kuswali katika kaburi la Imamu ´Aliy bin Abi Twaalib (‘Alayhis Salaam) ina ubora wa Swalah laki mbili.”(3)

Bali Shaykh wao ‘Abbaas Al-Kaashaaniy katika kitabu chake ‘MaswaabiyhulJinaan’ kapituka mipaka katika kuitukuza Karbalaa mpaka akasema: “Hapana shaka kwamba Karbalaa ndio sehemu takatifu zaidi katika Uislamu, na imepewa utukufu ambao haikupewa sehemu yoyote ardhini, na hii ni kwa mujibu wa dalili nyingi zilizopokewa kuhusu jambo hili, hivyo ikafanywa ndio ardhi ya Allaah iliyotukuzwa na kubarikiwa, na ni ardhi iliyonyenyekea, na ni ardhi iliyoteuliwa na ndio haram ya Allaah yenye baraka na amani, na ndio haram ya Mtume, na ndio kitovu cha Uislamu, na ni katika sehemu ambazo Allaah Anapenda kuombwa na kuabudiwa katika sehemu hizo, na ndio ardhi ambayo udongo wake ni tiba, hakika sifa hizi na nyinginezo zilizopo katika ardhi ya Karbalaa, hazipatikani katika sehemu yoyote ardhini, hata katika AlKa´abah.”(4)

Vilevile imekuja katika kitabu ‘Al-Mazaar’ cha Muhammad An-Nu’umaan, wenyewe wanamuita ‘Ash-Shaykhul-Mufiyd’ akielezea ubora wa Masjid AlKuufah: Imepokewa toka kwa Abu Ja’afar Al-Baaqir amesema: “Lau watu wangejua fadhila zinazopatikana katika Masjid Al-Kuufah basi wangeliuandalia matumizi na vipandwa kutoka sehemu mbalimbali ili kuuendea, hakika Swalah ya faradhi katika Msikiti huo ni sawa na Hijjah, na Swalah ya Sunnah ni sawa na `Umrah.”(5)

Vilevile imekuja katika kitabu hicho hicho katika mlango aliyouita ‘Yasemwayo wakati wa kusimama katika kaburi’ kwamba mwenye kumzuru Husayn anatakiwa kuashiria kwa mkono wake wa kuume, na aseme katika du´aa ndefu kabisa, miongoni mwake maneno yafuatayo: “Nimekujia kukuzuru, nikitaraji uthibitishwe unyayo wangu, na nina yaqini kwamba Allaah Mtukufu Anawaondolea waja Wake matatizo yao kupitia kwenu, na kwa sababu yenu anateremsha Rahma, na kupitia nyinyi anaizuia ardhi isiwadidimize watu wake, na kupitia nyinyi kayathibitisha majabali yake. Ninamuelekea Mola wangu kupitia kwenu ili mnikidhie haja zangu, na mnisamehe madhambi yangu.” (6)

Hebu tazama ndugu msomaji jinsi watu hawa walivyotumbukia katika ushirikina, kwa kumuomba asiyekuwa Allaah awakidhie haja zao, na kuomba kusamehewa madhambi yao kwa asiyekuwa Allaah, vipi wamefikia katika hali hii, na ilihali Allaah Anasema:

[Hakuna anayesamehe madhambi ila Allaah.]  [Al-´Imraan 03: 135].

Tunamuomba Allaah Atukinge na ushirikina. *

  •  1) Bihaarul-Anwaar 10/107.
  • 2) Bihaarul-Anwaar cha Al-Majlisiy 85/98.
  • 3) Minhaajus-Swalihiyn cha As-Sistaaniy 1/187.
  • 4) Maswaabiyhul-Jinaan cha ´Abbaas Al-Kaashaaniy uk. 360.
  • 5) Kitaabul-Mazaar cha Shaykh Al-Mufiyd uk. 20.
  • 6) Kitaabul-Mazaar cha Shaykh Al-Mufiyd uk. 99.

* MIONGONI MWA ITIKADI ZA MASHIA ‘Abdullaah Bin Muhammad As- Salafiy Uk / 32-33


Toa maoni yako

Begin typing your search above and press return to search.